"eti Single boy ya Alikiba amekopi"

Msanii anayedai kubiwa wimbo na Alikiba

MSANII chipukizi wa muziki wa kizazi kipya, Marius Rashid ameibuka na kudai kuwa, wimbo wake wa Single Boy umeibwa na msanii nyota wa muziki huo, Ali Kiba.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, msanii huyo ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Cos B alisema, aliutunga wimbo huo miezi mitano iliyopita.
Cos B alisema hakuwahi kuurekodi wimbo huo kwenye studio yoyote zaidi ya kumpatia Kiba kwa lengo la kumsaidia kuurekodi.
“Wakati nikihangaika kutafuta mfadhili ili anisaidie kuurekodi wimbo huo, nikakutana na Ali Kiba kwenye studio za G Records,”alisema Cos B.
“Baada ya kukutana naye, nilimuomba anisaidie nipate nafasi ya kurekodi kwenye studio hiyo, akaniomba nimwimbie kwanza wimbo wangu niliotaka kuurekodi,”aliongeza msanii huyo.
Cos B alisema baada ya kuuimba wimbo huo kwa mara ya kwanza, Kiba alitokea kuvutiwa nao na akamuomba auimbe kwa mara ya pili ili ausikilize tena.
“Wakati nikifanya hivyo, sikujua kwamba alikuwa akiurekodi wimbo huo maana alikuwa ameshika simu yake ya mkononi na kuibonyezabonyeza,”alisema.

Alipoulizwa kwa njia ya simu iwapo tuhuma hizo ni za kweli, Kiba aliomba kwanza apewe Cos B ili azungumze naye kabla ya kujibu swali hilo.
Alipobanwa zaidi na kuelezwa mazingira ya kuupata kwake wimbo huo kutoka kwa Cos B, Kiba alikana kumjua msanii huyo na kudai kuwa, hajawahi kuiba wimbo wake.
‘Huu wimbo ni wa kwangu na ingekuwa vizuri iwapo ningekutana na msanii huyo ili anieleze ni lini nilimwibia wimbo wake,’ alisema Kiba akionekana kuwa na hasira. 

Comments